- Mimea

Unaweza kufaidika na kuongeza pato kwa kuzalisha bamia

Sambaza chapisho hili

Bamia ni zao linalolimwa sana nchi za joto. Zao hili hutumika kama mboga inayoliwa matunda.

Asili ya mboga hii ni Afrika ya Kati na ya Mashariki, lakini kwa sasa zao hili limeenea katika sehemu nyingi za kitropiki, kama Visiwa vya Caribbean, Malaysia na Philipines.

Zipo aina nyingi za bamia, aina zile za kiasili nazo hutofautiana kulingana na eneo moja na lingine.

Matumizi

Bamia hupikwa pamoja na nyama, samaki au mboga nyingine.

Aidha majani yake pia huweza kuchumwa yakiwa bado machanga na kutumiwa kama mboga nyingine za majani.

Lishe

Zao la bamia lina virutubisho vingi ambavyo ni muhimu kwa miili yetu kama;

  • Madini ya chokaa ambayo hujenga meno na mifupa
  • Husaidia sehemu za viungo mbalimbali vya mwili kama sehemu za magoti, utumbo na macho

Udongo

Bamia humea na kukua vizuri kwenye udongo wenye rutuba ya kutosha na udongo usiotuamisha maji.

Aidha, kama ardhi haina rutuba ya kutosha, ni vyema kuweka mbolea ya mboji au samadi.

Hali ya hewa

Zao hili hustawi katika mita 1000 kutoka usawa wa bahari na haliwezi kuvumilia hali ya baridi kali.

Uoteshaji

  • Shamba la bamia ni vizuri lilimwe mapema kabla ya kuotesha bamia.

Mbegu za kuotesha

  • Mbegu bora zenye kutoa mavuno mengi zichaguliwe.
  • Mbegu za bamia huota kwa shida, mara nyingi huchukua siku nane hadi 12 kutokeza. Ili kurahisisha uotaji, inapendekezwa kulowekwa mbegu kwa muda wa siku moja kabla ya kuotesha ili kurahisisha uotaji.
  • Mbegu mbili zipandwe kwenye shimo moja.

Nafasi

Nafasi ya upandaji iwe ni sentimita 30 toka shimo hadi shimo na sentimita 50 toka mstari hadi mstari.

Kwa zile aina zinazorefuka sana iwe sentimita 40 kati ya shimo na shimo na sentimeta 70 kati ya mstari na mstari.

Palizi

Hakikisha shamba ni safi wakati wote kwa kuondoa magugu mara tu unapoona yamejitokeza.

Umwagiliaji

Iwapo unyevu wa ardhi hautoshi, inapendekezwa kutumia mojawapo ya njia za kumwagilia maji bustanini.

Wadudu waharibifu

Wapo wadudu wengi wanaoshambulia zao hili la bamia kama vile kimamba, funza wa vitumba na utitiri mwekundu.

Magonjwa

Magonjwa kama ukungu, ubwiri poda na kunyauka ndio huathiri zao la bamia hivyo ni vyema kuzuia kwa kufuata mzunguko wa mazao na kutumia dawa kulingana na ushauri wa wataalamu wa kilimo.

Mambo ya kuzingatia

  • Tumia mbegu bora
  • Panda kwa nafasi
  • Mwagilia maji ya kutosha
  • Palilia shamba vizuri na
  • Vuna kwa wakati unaotakiwa.

Uvunaji

  • Bamia huvunwa kabla ya kukomaa yaani zikiwa bado changa.
  • Kiasi cha kilo 8000 zaweza kupatikana katika ekari moja iwapo zitatunzwa vizuri.
  • Hakikisha unavuna bamia na kikonyo chake, kisu kinaweza kutumika kuvuna.

 

 

 

Maoni kupitia Facebook
Sambaza chapisho hili

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *