- Mifugo

Ugonjwa wa kiwele (mastitis)

Sambaza chapisho hili

Katika toleo lililopita tulizungumzia kwa ufupi kuhusu ugonjwa wa kiwele, madhara pamoja na dalili zake. Aidha tuliona jinsi ugonjwa huu unavyosababisha uvimbe, muwasho na joto kwenye kiwele cha mnyama na usababishwa na aina nyingi ya wadudu aina ya bakteria.

Katika toleo hili, tutamalizia mada hii kwa undani ili mfugaji aweze kufahamu namna ya kuzuia ama kukabiliana na ugonjwa huu mara endapo ng’ombe atakuwa amepata.

Njia zinazochangia ng’ombe kupata mastitis:

1.   Ng’ombe mwenyewe:

  • Vinasaba alivyonavyo ng’ombe vinavyomtofautisha na mwingine vinamchango mkubwa wa kumfanya asipate ugonjwa wa kiwele au aupate kirahisi ukilinganisha na mwingine.
  • Utoaji wake wa maziwa, ng’ombe anayetoa maziwa mengi hupata ugonjwa huu kirahisi pia
  • Mazingira ndani ya kiwele ni ya joto na virutubisho vingi na hivyo kutengeneza mazingira mazuri ya bakteria kuzalina kwa wingi na haraka.
  • Maumbile ya kiwele na chuchu huchangia uambukizwaji rahisi wa bakteria kulingana na yalivyokaa hasa yale yanayoning’inia chini na marefu kiasi cha kujigusa kwenye miguu ya ng’ombe
  • Ng’ombe kuwa na magonjwa mengine huchangia kupata ugonjwa wa kiwele.
  • Kupungua kwa kinga inayotokana na kuzaa au kufanyiwa upasuaji.
  • Lishe duni

2.Njia za ukamuaji:

  • Ukamuaji waweza kufanyika kwa njia ya mikono au mashine.
  • Ukamuaji unaofanywa na mikono hutegemea sana na umakini wa mkamuaji mwenyewe. Kama mkamuaji atakamua maziwa yote kwa ng’ombe hupunguza maambuki ya ugonjwa kiwele, la sivyo atasababisha ugonjwa. Usafi wa mkamuaji ni muhimu ili kuhakikisha haambukizi ugonjwa kutoka kwa ng’ombe mmoja kwenda mwingine.
  • Ukamuaji wa kutumia mashine ni mzuri lakini kama hewa haijawekwe kisahihi husababisha uharibifu kwenye chuchu na hivyo kuwa rahisi kwa bakteria wa ugonjwa wa kiwele kupenyeza.

3.   Mazingira ya ukamuaji:

  • Eneo analokamuliwa mnyama linapaswa kuwa safi, chuchu za mnyama zinapaswa kusafishwa kabla ya ukamuaji kuanza ili kuzuia bakteria wasiingie ndani ya kiwele.
  • Eneo analolala mnyama linapaswa kuwa safi ili kuepushe viwele na chuchu kuchafuka na mbolea inayobeba wadudu wengi wa magonjwa.
  • Mkamuaji anapaswa kuwa msafi na hata vyombo anavyokamulia viwe safi ili kuondoa mazingira ya kuzalisha bakteria wa ugonjwa huu

Bakteria wa ugonjwa wa kiwele wanaweza kutoka wapi?

  • Bakteria wa ugonjwa huu wanaweza kutoka
  • Kwenye kiwele cha ng’ombe aliye na ugojwa
  • Kwenye mazingira kama ng’ombe wanapolala, kwenye mbolea, kwenye udongo na maji yenye wadudu hawa.
  • Kuletwa na wanyama wapya walionunuliwa na kuingizwa kundini

Dalili za ugonjwa wa kiwele

Dalili za ugonjwa wa kiwele zimegawanyika katika makundi makubwa mawili; zinazoonekana kwa macho na zisizoonekana kwa macho.

 

1. Dalili zinazoonekana kwa macho

  • Kiwele huvimba, huwa na rangi nyekundu, cha moto na huwasha kusababisha ng’ombe ajikune, na huwa kigumu chote au baadhi ya maeneo.
  • Ng’ombe hukosa hamu ya kula na hunyong’onyea
  • Maziwa huwa yamevilia (vibonge bonge), hupoteza rangi yake na huweza kuwa na mchanganyiko wa damu au usaha

2.   Dalili zisizoonekana kwa macho

Hizi ni dalili zinazoonekana kwa kutumia kifaa maalumu kinachoangalia ongezeko la seli kwenye maziwa (CMT), kiifaa kinachotumiwa na mfugaji mwenyewe. Vipo vifaa vingine kama SCC vinavyoangalia ongezeko la seli kama dalili ya ugonjwa huu. Maziwa ya kila chuchu huwekwa sehemu yake na tambua yametoka chuchu ipi.

 

Matibabu ya ugonjwa wa kiwele

Ugonjwa wa kiwele unatibika na hasa matibabu yakifanywa mapema kabla ya ugonjwa kuwa sugu. Zipo aina mbalimbali za dawa zinazotumika kutibu ugonjwa huu.

Zipo dawa zinazowekwa kupitia mrija wa chuchu na zipo zinazochomwa kwenye mirija ya damu au kwenye myama. Wasiliana na Daktari wa eneo lako ili akuelekeze dawa inayofaa kwa mifugo yako.

Muhimu: Maziwa ng’ombe anaetumia dawa hayafai kwa binadamu, kwani yana athari kwa mwili wa binadamu.

 

IENDELEE IKAE KWENYE BOX KATIKA PG 3  CHINI AU RAW YA KULIA

 

Njia 10 za kuzuia ugonjwa wa kiwele

 

  1. Andaa ng’ombe wako vizuri kwa ukamuaji
  • Hakikisha chuchu za ng’ombe wako umezizamisha kwenye dawa maalumu ya kuzuia maambukizi
  • Kausha chuchu zako kwa kijitaulo (kitumike kimoja kwa kila ng’ombe) kabla ya kukamua au kuweka mashine.

2.              Uwe na mfumo mzuri wa ukamuaji

  • Vifaa vya ukanuaji lazima viwe na nafasi ya kutosha, vinafanya kazi vizuri na vinasafishwa vizuri kila wakati mara baada ya kutumiwa.
  • Kama unatumia mashine, hakikisha infanya kazi vizuri na andaa kiwele vizuri kabla ya kutumia mashine. hakikisha vikombe vya chuchu vimeoshwa vizuri na kukaushwa na hewa imewekwa kwa usahihi.

3.  Kamua kwa umakini na usahihi

  • Hakikisha unakamua maziwa yote na humumizi ng’ombe
  • Kama unatumia mashine pachika vikombe na ondoa kwa uangalifu ili usimuumize ng’ombe kwa kuweka hewa sahihi na kuzima hewa kabla na baada ya kuondoa chuchu.

4.  Chovya kila chuchu kwa kutumia dawa ya kuua wadudu mara umalizapo kukamua

  • Kuchovya chuchu kwenye dawa mara baada ya kukamua husaidia kuziba chuchu kwa muda wa masaa 6 hadi 8 ili kuzuia bakteria wasiingie ndani ya kiwele

5.  Weka utaratibu wa kuangalia ugonjwa kiwele usionekana kwa macho

 

  • Hakikisha unapima wanyama wako wote kuangalia uwepo wa ugonjwa wa kiwele usioonekana kwa macho kwa kutumia kifaa hiki hapa chini (CMT) na pia kwa kutumia kifaa kinachoangalia ongezeko la seli.
  • Tibu wanyama wote watakaoonyesha uwepo wa ugonjwa.

6.  Tibu wanyama wote wanaoonyesha ugonjwa kwa macho

  • Tutumia dawa utakayoshauriwa na mtaalamu wa mifugo wa eneo lako kwa uangalifu na kwa kufuata maelekezo kwenye kibandiko au ya mtaalamu wako.

7.  Tenga ng’ombe wenye ugonjwa

  • Ng’ombe yeyote mwenye ugonjwa atengwe na akamuliwe wa mwisho. Na yule mwenye ugonjwa sugu ikiwezekana auzwe kwani anaongeza gharama bila faida na tena hueneza ugonjwa kwa ng’ombe

8.  Weka dawa ya kumkausha ng’ombe unapomkausha

  • Dawa ya kumkausha ng’ombe ni muhimu sana itumike kwani itasaidia kuua wadudu ili aingie awamu nyingine ya ukamuaji akiwa hana wadudu wa ugonjwa
  • Uponyaji wake ni mara mbili ya ile inayotumika wakati wa ukamuaji

9.  Siku zote hakikisha ng’ombe wako ni wasafi

  • Usafi wa ng’ombe ni muhimu ili kuzuia bakteria wa udongoni na kwenye mbolea wanaosababisha ugonjwa huu.
  • Hakikisha kiwele hakichafuliwi na udongo au mbolea, maeneo ya kuzalia yawe safi na yamewekwa malalia.
  • Banda liwe safi lisilotuamisha maji wala kutengeneza matope

10.  Tunza na lisha mifugo yako vizuri

  • Siku zote hakikisha mifugo yako inakula vizuri, inapewa chakula cha ziada na madini ili kusadia kujenga kinga ya mwili itakayosaidia kupambana na magonjwa.

KUMBUKA: Zingatia kufuata kanuni za chakula na usafi ili kupunguza asilimia kubwa ya maambukizi.

Kwa mawasiliano Zaidi, wasiliana na Augustino Chengula wa Chuo kikuu cha kilimo  (SUA) Morogoro   kwa simu namba xxxxxxx

Maoni kupitia Facebook
Sambaza chapisho hili

2 maoni juu ya “Ugonjwa wa kiwele (mastitis)

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *