Tanzania imeendelea kujidhihirisha kuwa eneo lenye fursa kubwa kwa uwekezaji na biashara katika sekta ya kilimo barani Afrika, huku kampuni, wawekezaji, wakulima na wadau wengine wakikutana katika 10th Global Africa Agri Expo na 3rd Future Food and Livestock Expo yaliyofanyika katika Viwanja vya Sabasaba, Dar es Salaam.
Ikiwa ni siku ya pili, maonyesho hayo yameendelea kuwaweka pamoja wadau kutoka ndani na nje ya Tanzania, yakitoa nafasi ya kuonyesha bidhaa na teknolojia za kilimo, pamoja na kujenga uhusiano kati ya kampuni, wafanyabiashara, wakulima na watunga sera.

Akizungumza wakati wa maonyesho hayo, Tahir Abdul Bari, CEO na Managing Director wa CAP Group, kampuni inayoandaa maonyesho hayo, alisema Tanzania imechaguliwa kuwa mwenyeji wa toleo hili kutokana na uwezo wake mkubwa katika kilimo na nafasi yake kama lango muhimu la biashara katika Afrika Mashariki.
“Tunaona fursa kubwa sana katika sekta ya kilimo nchini Tanzania. Tanzania ni moja ya lango muhimu la biashara katika ukanda wa Afrika Mashariki,” alisema Abdul Bari.
Kwa mujibu wa Abdul Bari, maonyesho hayo hayalengi tu kuonyesha bidhaa na teknolojia, bali pia kuunganisha kampuni za kimataifa na wafanyabiashara wa ndani, wakulima na watunga sera.
Lengo, alisema, ni kuwezesha uwekezaji na ushirikiano wa muda mrefu, huku sera na mipango ya serikali katika kilimo, mifugo, uvuvi na sekta nyingine zinazohusiana na uzalishaji wa chakula ikiendelea kuvutia kampuni zinazotafuta fursa za uwekezaji barani Afrika.
Suluhisho katika mnyororo mzima wa kilimo
Kwa kampuni zinazotoa teknolojia na huduma za kilimo, fursa hazipo katika uzalishaji pekee, bali katika hatua mbalimbali za mnyororo wa thamani.
Fauzia Ally, mwakilishi wa AgriCom Africa, alisema kampuni inalenga kumpa mkulima suluhisho katika hatua tofauti za shughuli za kilimo, kuanzia maandalizi ya shamba hadi baada ya mavuno.
Huduma hizo zinahusisha utayarishaji wa mashamba, utunzaji wa mashamba na mazao, uvunaji, uchakataji na usafirishaji.
“Tunatoa suluhisho kwa mkulima katika mnyororo mzima wa shughuli za kilimo,” alisema Ally.
Mbali na vifaa na huduma zinazohusiana na uzalishaji, kampuni hiyo pia inaendelea kutoa huduma baada ya mauzo, ikiwa ni pamoja na upatikanaji wa vipuri na usimamizi wa huduma za warranty.
Kwa wakulima, huduma za aina hii zinaweza kuwa muhimu katika kuhakikisha kuwa uwekezaji katika teknolojia na vifaa unaendelea kutoa thamani hata baada ya ununuzi.
Umwagiliaji kuongeza ufanisi wa uzalishaji
Teknolojia ya umwagiliaji pia imepewa nafasi katika maonyesho hayo, huku kampuni zikionyesha mifumo inayolenga kuongeza ufanisi wa matumizi ya maji na kusaidia wakulima kukabiliana na changamoto zinazohusiana na uzalishaji.
Akizungumza katika maonyesho hayo, Ahmed Riyad, Export Manager wa Hatinahi Company for Modern Irrigation Systems, alisema kampuni inatumia ushiriki wake katika maonyesho hayo si kwa ajili ya kuonyesha bidhaa pekee, bali pia kujenga ushirikiano wa kimkakati unaozingatia uaminifu, ubora na maendeleo endelevu ya kilimo.
Bidhaa zinazoonyeshwa na kampuni hiyo ni pamoja na hoses, tape hoses, mifumo ya umwagiliaji na sprinkler systems, ambazo zimeundwa kwa ajili ya matumizi katika kilimo cha kisasa.
Riyad alisema kampuni hiyo inazingatia viwango vya kimataifa katika bidhaa zake na inalenga kuhakikisha kuwa mifumo hiyo inaweza kutumika katika mazingira mbalimbali.
Jukwaa la kujenga ushirikiano
Ushiriki wa kampuni kutoka sekta mbalimbali unaonyesha kwamba maendeleo ya kilimo yanahitaji zaidi ya uzalishaji wa mazao shambani. Yanahitaji pia teknolojia, huduma, miundombinu, masoko, uwekezaji na ushirikiano kati ya wadau.
Kwa kuwakutanisha wakulima, wazalishaji, wafanyabiashara, wawekezaji, kampuni za kimataifa na watunga sera, Global Africa Agri Expo inatoa jukwaa la kujenga mahusiano ambayo yanaweza kusaidia kuchochea uwekezaji na matumizi ya teknolojia mpya katika kilimo.



